TWCC yawahimiza Wanawake Wajasiriamali kushiriki Tuzo za Viwanda na Biasahara, kufanya Maonyesho Siku ya Wanawake Duniani

Na Isack Magessa

Chama cha Wanawake Wafanyabiashara Tanzania (TWCC) kimewahimiza wanawake wajasiriamali na wafanyabiashara kushiriki katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ambayo yanaambatana na Maonyesho ya Bidhaa mbalimbali na Utoaji Tuzo kuanzia Machi 9 hadi 11 mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam Mkurugenzi wa TWCC,Mwajuma Hamza amesema katika sherehe hizo zitakazofanyika katika viwanja vya  mlimani city na baadaye kutolewa kwa tuzo katika ukumbi huo Macchi 11,2023 zenye lengo la kutambua na kuheshimu wanawake waliofanikiwa na wale wanaochipukia katika sekta za viwanda na biashara.

Amebainisha kuwa malengo mengine ya kutolewa kwa tuzo hizo ni pamoja na kujenga imani juu ya ujasiriamali na kuhamasisha wanawake wa vizazi vijavyo kuwekeza na kujishughulisha katika shughuli za viwanda na biashara,pamoja na kusheherekea mafanikio wanayoyapata wanawake katika sekta za viwanda na biashara hapa nchini.

Mwajuma Hamza amesisitiza kuwa tuzo hizo ambazo zinatolewa kwa mara ya tatu pia zinalenga kuonesha mchango wa mwananmke mjasiriamali katika kukuza uchumi wa nchi kwa kuchoche maendeleo ya jamii.

"wanawake ni nguzo muhimu katika maendeleo ya jamii yoyote na kwamba wanawake wana uwezo wa kufanya mapinduzi makubwa katika sekta ya viwanda na biashara endapo wataaminiwa na kupewa nafasi hiyo"aliongeza 

 Ameishukuru serikali kwa kuendelea kuboresha mazingira ya biashara nchini ambapo wanawake wengi wameweza kuanzisha biashara na viwanda vidogo ambavyo vimewaongezea vipato,kuzalisha ajira pamoja na kuchangia katika kukuza uchumi.

"Kipekee kabisa ninamshukuru Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kufungua nchi na kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini,sisi wanawake tumejipanga kikamilifu katika kutumia fursa vizuri kupitia wiki hii ya viwanda ya wanawake ndipo tunapata nafasi ya kujitathmini na kuweka mikakati ya kuendeleza biashara zetu"alisisitiza Bi Mwajuma Hamza

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkazi  wa TradeMark Africa (TMA), Monica Hangi ambao ndiyo wadhamini wakuu wa tuzo hizo chini ya miradi wa kujengea wanawake uwezo wa kufanya biashara Tanzania amesema TMA imetenga kiasi cha Sh Bilioni nne kwa ajili ya mradi huo wa kuwawezesha wanawake kufanya biashara.

 Ameongeza kuwa TradeMark Africa imeamua kudhamini tuzo hizo za wanawake kupitia TWCC kwa lengo kubwa la kuhakikisha biashara za wanawake zinakuwa na kuleta tija kwa Taifa kwani tuzo hizo zimekuwa zikitoa chachu kwa wanawake wengi kutamani kuingia kwenye biashara.

"Wapo wanawake wengi wanaojifunza kupitia wale waliofanikiwa na hii ndiyo maana halisi ya hizi tuzo kuwatangaza wale wote waliofanikiwa na wanaofanya vizuri kibiashara ili wengine waweze kujifunza"Ameongeza Mkurugenzi Mkazi wa TMA Monica Hongi

Comments